Michezo ya Olimpiki ya Rio 2016 kufunguliwa rasmi, Afrika ina matarajio makubwa
Makala ya 31 ya michezo ya Olimpiki ya Rio nchini Brazil inafunguliwa rasmi hii leo, katika sherehe zitakazofanyika kwenye uwanja wa michezo wa Maracana ambao pia ulitumika kwenye fainali ya kombe la dunia mwaka 2014.
Imechapishwa:
Wanamichezo kutoka mataifa 206 pamoja na timu ya wanamichezo ambao ni wakimbizi, wanashiriki michezo ya mwaka huu inayofanyika Brazil, ambapo watashindana katika michezo 28 na kutazamwa na mabilioni ya watu duniani.
Kuelekea michezo ya mwaka huu, iligubikwa na kashfa kubwa ya matumizi ya dawa za kusisimua misuli kwa nchi ya Urusi pamoja na kuenea kwa maambukizi ya virusi vya Zika, vinavyosababishwa na mbu.
Suala la usalama, hali ya kisiasa miundo mbinu na viwanja ni masuala mengine yaliyogubika michezo ya mwaka huu.
Hata hivyo pamoja na sintofahamu zote hizi, hatimaye sasa michezo hii inaanza rasmi.
Hii ni michezo ya makala ya 31 ya Olimpiki, lakini ni ya 28 kuandaliwa ukiacha ile ya mwaka 1916, 1940 na 1944 ambayo haikufanyika kutokana na vita vya dunia.
Inakadiriwa kuwa watu karibu bilioni 3 duniani watatazama ufunguzi wa michezo ya mwaka huu, ambapo imechukua miaka mitano kuitengeneza, huku wachezaji 300, watu wa kujitolea elfu 5 na mavazi zaidi ya elfu 12.
Afrika pia inawakilishwa ipasavyo kwenye michezo ya mwaka huu, huku wanariadha wa Kenya, Ethiopia, Algeria, Afrika Kusini na Tanzania wakitarajiwa kujaribu kulitoa bara la Afrika kimasomaso.