Keshi kuzikwa kinyume na wito wa serikali
Mazishi ya Stephen Keshi, aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya soka ya Nigeria, yameanza leo Alhamisi katika mji wa Benin katika jimbo la Edo.
Imechapishwa:
Familia ya Keshi imeamua kuendelea na taratibu za mazishi licha ya serikali kutaka mazishi hayo kufanyika baada ya michezo ya Olimpiki inayoonza wiki ijayo.
Keshi alifariki dunia mapema mwezi uliopita akiwa na umri wa miaka 54 na mazishi yake yamekuwa yakicheleweshwa kwa sababu za kifedha.
Atakumbukwa kuwa kocha na mchezaji wa timu ya taifa Super Eagles lakini pia kuiongoza nchi yake kushinda taji la mataifa bingwa barani Afrika mwaka 2013.
Mechi maalum imeandaliwa kumkumbuka Keshi ambaye amekuwa shujaa wa mchezo wa soka nchini humo.
Wakati wa uhai wake, aliwahi pia kuiongoza Nigeria kucheza katika kombe la dunia mwaka 2014 nchini Brazil.
Mbali na nchi yake ya Nigeria, Keshi aliwahi pia kuwa kocha wa timu taifa ya Mali na Togo.