Hofu ya usalama yazidi kutanda Ufaransa kuelekea Euro 2016
Licha ya kuweka mikakati mizuri ya kiusalama kabla, wakati na baada ya fainali za kombe la Ulaya "Euro" inayotarajiwa kuanzaz kutimua vumbi Ijumaa ya wiki hii nchini Ufaransa, taifa hilo bado linaendelea kukumbwa na hofu ya kutekelezwa kwa mashambulizi ya kigaidi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Serikali ya rais Francois Hollande ilitangaza hali ya hatari kwenye miji kadhaa nchini humo baada ya mashambulizi ya mwaka uliopita jijini Paris, ikiwa ni pamoja na kuruhusu polisi kuvamia na kufanya upekuzi kwenye nyumba za watu wanaotuhumiwa kwa ugaidi.
Lakini licha ya hatua hizi, bado nchi hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa ya kuwadhibiti na kuwafuatilia raia wake wanaorejea kutoka nchini Iraq na Syria, ambapo walisafiri kwa kutumia pasi bandia huku kuongezeka kwa idadi ya wakimbizi ikiwa ni kitisho kikubwa.
Mwanzoni mwa juma hili, rais Hollande akizungumza na chombo kimoja cha habari nchini humo, alikiri kuhusu uwepo kitisho kilichopo cha kutekelezwa kwa mashambulizi ya kigaidi kuwalenga raia wanaowasili nchini humo kushuhudia michuano ya Euro.
Rais Hollande amesema kuwa, maofisa usalama nchini humo wanazotaarifa za uhakika kuhusu kuwepo kwa kitisho cha kutekelezwa kwa shambulizi la kigaidi kwenye baadhi ya miji ambayo itakuwa wenyeji wa mechi za kombe la Euro.
Ufaransa pia imetangaza kusambaza zaidi ya askari elfu 99 kwenye miji karibu zaidi ya 10 kwa lengo la kudhibiti hali ya usalama na kufanya upekuzi wa kina kwenye viwanja ambavyo vitatumiwa na mashabiki.
Polisi na wanajeshi wamepewa mamlaka ya kufanya ukaguzi wa kina kwa mashabiki watakao kuwa wanaingia uwanjani na wakati mwingine kukagua hata hoteli ambazo mashabiki watakuwa wanafikia.
Haya yanajiri wakati huu ambapo hapo jana, kokosi maalumu cha kupambana na ugaidi nchini Ukraine, kikifanikiwa kumkamata raia wa Ufaransa aliyekutwa na vifaa mbalimbali vya kivita zikiwemo bunduki, bastola, mabomu ya kutengeneza na unga wa kutengenezea mabomu.
Ukraine inasema kuwa raia huyo alikuwa amepanga kufanya mashambulizi kwenye zaidi ya maeneo 15 kwenye nchi za Ulaya, na kwamba michuano ya Euro nchini Ufaransa ilikuwa iko kwenye mipango ya mtuhumiwa huyo.
Hata hivyo Ufaransa na nchi nyingine wanachama za Umoja wa Ulaya wameapa kukabiliana na kitisho chochote cha ugaidi ili kuifanya michuano ya Euro kutumika kama kiungo muhimu cha kukabiliana na ugaidi.