Manchester City kukutana na Chelsea hatua ya tano michuano ya FA nchini Uingereza
Klabu ya Chelsea ya nchini Uingereza imefanikiwa kusonga mbele hatua ya tano ya michuano ya kombe la FA baada ya hapo jana kupata ushindi, na sasa itakutana na Manchester City.
Imechapishwa:
Katika michuano ya mwaka huu hatua ya mzunguko wa tano, klabu ya Shrewsbury ndio klabu pekee ya daraja la chini iliyofanikiwa kuingia kwenye hatua ya tano ya kombe la FA, na sasa itakutana na Manchester United.
Arsenal wao baada ya kusonga mbele kwenye hatua ya tano, sasa watakutana na Hull City ikiwa ni kama marudio ya mechi ya fainali ya mwaka 2014 ambapo timu hizi zilikutana kwenye hatua ya fainalia.
Crystal Palace wenyewe watakuwa wageni wa klabu ya Tottenham Hotspurs huku timu ya Bournemouth ikitarajiwa kuikaribisha Everton kwenye mtanange mwingine utakaozikutanisha timu zinazoshiriki ligi kuu ya Uingereza.
Mechi hizi zote zinatarajiwa kupigwa tarehe 19 na 22 ya mwezi February mwaka huu.
Mechi nyingine za hatua ya tano ya kombe la FA, ni pamoja na Watford ambao watawakaribisha Leeds United, wakati Reading watacheza na mshindi wa mechi ya marejeano kati ya West Brom na Peterborough, huku Blackburn ikiwa wenyeji wa vijogoo vya jiji Liverpool au West Ham.
Mechi ambayo inasubiriwa kwa hamu na gamu ni ile itakayoikutanisha timu ya Chelsea na Manchester City, ambapo kocha mkuu wa Chelsea, Guus Hiddink anasema itakuwa ni mechi ya kukata na shoka.
Mechi nyingine ni ile kati ya Arsenal na Hull City ambao watakutana kwa mara ya tatu mfululizo, ambapo mara ya mwisho Arsenal waliifunga Hull City kwa mabao 2-0 katika michuano ya mwaka uliopita.
Mechi zenyewe ni kama ifuatavyo:-
Chelsea v Manchester City
Reading v West Brom au Peterborough
Watford v Leeds United
Shrewsbury Town v Manchester United
Blackburn v Liverpool au West Ham
Tottenham v Crystal Palace
Arsenal v Hull
Bournemouth v Everton