Brazil na Colombia zafuzu hatua ya robo fainali
Brazil imefuzu katika hatua ya robo fainali ya michuano ya soka ya kombe la dunia baada ya kuwashinda Chile kwa mabao 3 kwa 2 kupitia mikwaju ya penalti Jumamosi usiku.
Imechapishwa:
Mchuano huo ulilazimika kufikia hatua ya kupigwa penalti baada ya timu zote mbili kutoka sare ya bao 1 kwa 1 katika muda wa kawaida na ule wa ziada.
David Luiz aliipa Brazil bao la ufunguzi katika dakika ya 18 ya mchuano huo kabla ya Alexis Sanchez kuishawazishia timu yake katika dakika ya 32 .
Kipa wa Brazil Julio Cesar ndiye aliyekuwa mchezaji bora katika mchuano huo kwa kuikoa timu hiyo kwa kuokoa penalti mbili.
Cesar aliokoa penalti ya Mauricio Pinilla na Alexis Sanchez, huku wao Brazil wakifunga penalti 3 katika mchuano huo mgumu.
Penalti zilifungwa na David Luiz , Marcelo na Neymar.
Mbali na Brazil, James Rodriguez wa Colombia aliifungia timu yake mabao mawili katika dakika ya 28 na 50 na kuwabandua nje Uruguay katika michuano hii.
Rodriguez anakuwa mchezaji wa kwanza kufunga bao katika kila mechi katika michuano hii na hadi sasa, ni mfugaji bora akiwa na mabao 5, akifuatwa na Neymar wa Brazil na Lionel Messi wa Argentina ambao wana mabao 4.
Hii ndio mara ya kwanza katika historia ya Colombia kufuzu katika hatua ya robo fainali.
Brazil itamenyana na Colombia katika hatua ya robo fainali, siku ya Ijumaa juma lijalo.