Algeria yashangilia kufuzu hatua ya 16 bora, Ghana warudi nyumbani
Maelfu ya raia wa Algeria bado wanasherehekea kufuzu kwa timu yao ya taifa alimaarufu kama “The Desert foxes” katika hatua ya 16 bora katika michuano ya soka ya kombe la dunia inayoendelea nchini Brazil.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Algeria walifuzu baada ya kutoka sare ya bao 1 kwa 1 na Urusi Alhamisi usiku katika mchuano wa kutamatisha kundi lao.
Urusi ndio iliyokuwa ya kwanza kupata bao katika kipindi cha kwanza cha mchuano huo, kabla ya Algeria kusawazisha kupitia Islam Slimani katika kipindi cha pili cha mchuano huo.
Algeria itamenyana na Ujerumani katika hatua ya mwondoano siku ya Jumatatu juma lijalo.
Kufuzu kwa Algeria kumewakumbusha wengi mwaka 1982 ambapo Ujerumani Magharibi ilitoka sare makusudi na Austria na kuwanyima nafasi Algeria kufuzu katika hatua ya 16 bora.
Jijini Paris, polisi wanasema wamewakamata zaidi ya raia 70 wa Algeria ambao walikuwa wanafanya fujo na kuiba bidhaa baada ya Algeria kufuzu.
Wawakilishi wengine wa Afrika Ghana, walibanduliwa nje ya michuano hiyo baada ya kushindwa kupata ushindi dhidi ya Ureno ambao waliwafunga mabao 2 kwa 1.
Licha ya Ureno kupata ushindi huo, haikufuzu kwa sababu ilifanya vibaya katika michuano yake miwili ya ufunguzi.
Mataifa ya Ujerumani na Marekani yamefuzu licha ya Marekani kufungwa na Ujerumani bao 1 kwa 0.
Hii ndio mara ya kwanza tangu kuanza kwa michuano ya soka ya kombe la dunia mwaka 1930 kwa timu mbili za Afrika kufuzu katika hatua ya mwondoano.
Asamoh Gyan wa Ghana licha ya timu yake kuondolewa katika michuano hiyo, anaweka Historia kuwa mchezaji wa kwanza wa Afrika kufunga mabao 6 katika kombe la dunia na kuvunja rekodi ya Roger Milla kutoka Cameroon aliyefunga mabao 5 miaka ya tisini.
Nacho kikosi cha Nigeria hakijahudhuria mazoezi siku ya Ijumaa kwa madai kuwa wachezaji hawajalipwa marupurupu yao.
Wachezaji wa Super Eagles wanadai marupurupu yao baada ya kufika katika hatua ya 16 bora.
Kikosi cha Super Eagles chini ya kocha Stephen Keshi walistahili kufanya mazoezi katika mji wa Campinas lakini hawakusafiri kwa sababu walikuwa kikaoni kujadili suala hilo.
Nigeria wanajiandaa kumenyana na Ufaransa katika hatua ya mwondoano siku ya Jumatatu juma lijalo, baada ya kumaliza wa pili katika kundi lao kwa alama 4.
Hii sio mara ya kwanza kwa Nigeria kugomea mazoezi kwa sababu ya marupurupu.
Timu nyingine ya Afrika ambayo ilijikuta katika hali hii ni pamoja Cameroon na Ghana ambao tayari wamebanduliwa nje ya michuano hii.
Ijumaa ni siku ya mapumziko na hii ndio ratiba ya michuano ya mwondoano kuanzia Jumamosi hii:
Jumamosi tarehe 28 Juni 2014
Brazil Vs Chile
Colombia Vs Uruguay
Jumapili tarehe 29 Juni 2014
Uholanzi Vs Mexico
Costa Rica Vs Ugiriki
Jumatatu tarehe 30 Juni 2014
Ufaransa Vs Nigeria
Ujerumani Vs Algeria
Jumanne tarehe 1 Julai 2014
Argentina Vs Uswizi
Ubelgiji Vs Marekani