Bayern Munich yaifanyia kweli Real Madrid, leo ni kati ya FC Barcelona na Chelsea
Nusu fainali ya kwanza ya kombe la ligi ya mabingwa barani Ulaya imeanza kupigwa hapo jana ambapo kulikuwa na mchezo mmoja kati ya FC Bayern Munich waliokuwa wenyeji wa Real Madrid ya Uhispani.
Imechapishwa:
Mchezo huo ambao ulipigwa kwenye dimba la Allianz Arena ulikuwa wa kusisimua kwa muda wote wa mchezo huku Bayern Munich akionekana kulisakama lango la Madrid kwa muda wote wa mchezo.
Katika mechi hiyo Bayern Munich walifanikiwa kuchomoza na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya vijana wa Madrid na kuufanya mchezo wa marejeano juma moja lijalo kuwa usiotabirika kwa timu zote mbili.
Bayern ndio waliokuwa wa kwanza kuandika bao katika dakika ya 17 kupitia kwa Frank Ribery kabla ya Mesut Ozil kuisawazishia timu yake bao katika dakika ya 53.
Bayern walipata bao la ushindi katika dakika ya 90 ya mchezo likifungwa na Mario Gomez na kuzamisha jahazi la Madrid ambapo kocha wake mkuu Josee Mourinho amesema walizembea na hivyo bayern walistahili kushinda.
Nusu fainali nyingine ya ligi hiyo itachezwa hii leo kwenye dimba la Stamford Bridge pale mabingwa watetezi wa kombe hilo FC Barcelona watakapokuwa wageni wa Chelsea ambayo imezinduka na wimbi la ushindi.
Makocha wa timu zote mbili wamejigamba kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo lakini wakikiri pia mchezo huo kuwa mgumu kwa timu zote mbili.