Baraza la Usalama kutathmini mpango wa amani wa Marekani kwa Mashariki ya Kati
Baraza la Usama la Umoja wa Mataifa linatarajia leo Jumanne kupigia kura mpango wa amani wa Marekani kwa Mashariki ya Kati. Hata hivyo Palestina inaendelea kupinga mpango huo ikibaini kwamba ni mpango usiokuwa na manufaa yoyote kwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Kiongozi wa mamalaka ya Palestina Mahmoud Abbas anatarajia kushiiriki kikao hiki cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Marekani imetishia kufuta msaada wa kifedha kwa nchi ambayo haitaunga mkono mpango huo; Lakini nchi nyingi za Afrika tayari zimeonyesha msimamo wao wa kutofurahishwa na mpango huo.
Viongozi wa mataifa ya Afrika ambao walikutana jijini Addis Ababa nchini Ethiopia, katika kikao chao cha wakuu wa nchi, walimshutumu rais wa Marekani Donald Trump kuhusu mpango aliotoa hivi karibuni kuhusu amani ya Mashariki ya Kati.
Wakuu hao walisema mpango huo haukubaliki na unaipendelea Israel na kuionea Mamlaka ya Palestina, na hivyo unakwenda kinyume na maamizio ya Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa kuhusu namna ya kutatua mzozo kati ya Israel na Palestina.
Mwenyekiti mpya wa Umoja wa Afrika, rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, alisema mapendekezo ya Marekani ni kitendo cha ubaguzi kama ilivyokuwa nchini Afrika Kusini wakati wa kipindi cha ubaguzi wa rangi.