Trump na Erdogan wazungumza kuhusu uamuzi wa Marekani kuondoa jeshi lake Syria
Rais wa Marekani Donald Trump amesema amezungumza kwa simu na mwenzake wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan, kuhusu kuondolewa kwa tararibu kwa wanajeshi wa Marekani nchini Syria.
Imechapishwa:
Aidha, amesema wamezungumzia kuhusu vita dhidi ya Islamic State, na ushirikiano wa Marekani na Uturuki nchini Syria, katika vita dhidi ya ugaidi.
Rais Tayyip naye amesema kuwa wamejadiliana mambo mengi ikiwemo pia namna ya kuimarisha biashara kati ya nchi hizo mbili.
Mazungumzo haya yamefanyika wakati huu Wizara ya ulinzi ya Marekani ikisema,tayari agizo la kuondolewa kwa wanajeshi wa Marekani nchini Syria, limeshatiwa saini.
Wakati huo huo shughuli za serikali zinatarajiwa kuendelea kukwama nchini Marekani, hadi mwezi Januari mwaka 2019, baada ya Maseneta kushindwa kupitisha bajeti muhimu ya fedha.
Hali hii ilianza kushuhudiwa, baada ya Maseneta wa Democratic kukataa kupitisha bajeti hiyo ambayo pia rais Donald Trump alitaka Dola Bilioni 5 zitumiwe kujenga ukuta katika mpaka na Mexico.
Hata hivyo, rais Trump ametetea uamuzi wake na kusema ni kwa sababu za kiusalama.