Mauaji ya Khashoggi: Kauli ya Saudi Arabia yaibua maswali mengi
Nchi ya Saudi Arabia sasa inasema kuwa mauaji ya mwandishi wa habari Jamal Khashoggi yanaonekana kuwa yalipangwa na hii ni kutokana na taarifa walizopewa na Uturuki, wakijiweka kando na matamshi yao ya awali kuwa alikufa baada ya kupigana kwenye ubalozi wake mjini Instanbul.
Imechapishwa:
Kauli hii mpya ya Saudi Arabia inaibua maswali zaidi kuhusu nia ya awali ya utawala wa Riyadh ambao ulikana kuhusika katika mauaji yake, mauaji ambayo rais wa Marekani Donald Trump anasema waliojaribu kuficha wameingia katika historia ya kuwa na mipango mibaya.
Katika hatua nyingine mtoto mkubwa wa kiume wa Khashoggi amewasili nchini Marekani baada ya kuruhusiwa kutoka nje ya nchi yake na utawala wa Riyadh ambao awali ulikuwa umemzuia kutoka kutokana na ukosoaji wa baba yake kwa Serikali.
Hata hivyo licha ya utawala wa Saudi Arabia kukiri kuhusu mwanahabari huyo kuuawa kwenye ubalozi wake, bado inakabiliwa na shinikizo kubwa kutoka jumuiya ya kimataifa ambayo inataka majibu ya kuridhisha kuhusu kilichotokea na mahali mabaki ya mwili wa Khashoggi yalipo.
Wakati huo huo wabunge wa Umoja wa Ulaya wameomba Saudi Arabia ichukuliwe vikwazo kutokana na kisa cha mauaji ya mwandishi wa habari Jamal Khashoggi.