Umoja wa Mataifa: Tunasikitishwa na mapigano yanayoendelea Syria
Jeshi la Syria, limewashambulia tena wapinzani wa rais Bashar Al Assad katika ngome yao ya Ghouta Mashariki, baada ya kushuhudiwa kwa usitishwaji wa mapigano kwa muda mfupi jana Jumanne.
Imechapishwa:
Serikali ya Urusi ambayo inaisaidia Syria, imesema, kusitishwa kabisa kwa mapigano katika ngome hiyo ya upinzani itategemea iwapo wapinzani wataacha mashambulizi.
Kwa sasa Syria, imetangaza kuwa, mashambulizi yatasitishwa kati ya saa tatu asubuhi na saa nane mchana kila siku kwa lengo la kuruhusu misaada ya kibinadamu kuwafikia waathiriwa.
Licha ya kupitishwa kwa azimio la Umoja wa Mataifa kusitishwa kwa mapigano kwa muda wa siku 30, yameendelea na kusababisha vifo vya raia wasiokuwa na hatia.
Wakati huo huo Umoja wa Mataifa umesema kuwa mapigano yanayoendelea yamezuia kusambaza misaada katika eneo la Ghouta mashariki linaloshikiliwa na waasi.