Kundi la IS lakiri kuhusika na shambulio la Kabul
Wapiganaji wenye silaha wamevamia kambi ya mafunzo ya idara ya usalama wa taifa nchini Afghanistan iliyoko mjini Kabul, shambulizi lililotekelezwa na wapiganaji wa kiislamu wa Islamic State, shambulio lililodumu kwa saa kadhaa.
Imechapishwa:
Vyombo vya usalama vilikabiliana na wapiganaji hao kwenye eneo ambalo ujenzi ulikuwa ukiendelea ndani ya kambi ya idara ya usalama wa taifa kabla ya kufanikiwa kuwaua wapiganaji wawili.
"Walikuwa wamejificha kwenye majengo yaliyokuwa yanaendelea kujengwa, tulilipua majengo hao na kuwaua wawili kati ya watatu," amesema afisa mmoja wa polisi aliyehusika kwenye operesheni hiyo.
Msemaji wa polisi mjini Kabul Basir Mujahid amesema kuwa polisi wawili walijeruhiwa katika makabiliano hayo na kwamba hakukuwa na madhara kwa raia wa kawaida.
Wakati wa makabiliano haya njia kuu za kuingia kwenye eneo hilo zilifungwa na mamia ya polisi na wale wa idara ya usalama walianza kukabiliana nao.
Ripota wa shirika la habari la AFP ambaye alikuwa amezuiwa kwenye eneo lenye umbali wa kilometa karibu moja na eneo la tukio anasema aliona magari ya wagonjwa na mamia ya wanajeshi na polisi wakielekea kwenye eneo la tukio.
Kundi la Islamic State limekiri kuhusika kwenye shambulio hilo.
Jiji la Kabul kwa miezi ya hivi karibuni limeshuhudia mashambulizi mabaya zaidi kuwahi kushuhudiwa dhidi ya raia wakati huu wanamgambo wa Taliban wakiendelea kutekeleza mashambulizi.