UNHCR yasitisha zoezi la kuwarudisha nyumbani raia wa Cote d'Ivoire walioko nchini Liberia
Maafisa wa Umoja wa Mataifa walio nchini Liberia wamesema kuwa wamesitisha kwa muda zoezi la kuwarudisha nchini Cote d' ivoir maelfu ya Wakimbizi kufuatia kukosekana kwa hali ya usalama katika eneo la karibu na mpaka wa nchi hiyo na Liberia.
Imechapishwa:
Maafisa kutoka Shirika linalohudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa wamesema kuwa Msafara wa watu waliokuwa wakirudishwa Cote d Ivoire watarejea nchini Liberia kwa kuwa hali ya usalama si nzuri nchini mwao.
Zaidi ya watu laki moja na hamsini raia wa Cote d Ivoire walikimbilia nchini Liberia wakati wa machafuko ya baada ya uchaguzi mwaka 2010, ambapo zaidi ya watu elfu sitini bado wako nchini liberia.
Baada ya mgogoro wa Cote d ivoire, wapiganaji wengi waliokuwa wakimuunga mkono Kiongozi wa zamani, Laurent Gbagbo walikimbilia nchini Liberia ambako wanaaminika kufanya mashambulizi mara kadhaa katika eneo la mpaka wa cote d ivoire na Liberia.
Hivi karibuni Umoja wa Mataifa uliripoti kuhusu kutoridhishwa na hali ya usalama kwenye mipaka ya nchi hizo mbili ambapo baadhi ya wapiganaji wamekuwa wakitekeleza mashambulizi dhidi ya wafanyakazi wake na wanajeshi wa Umoja huo wanaolinda amani nchini humo.