Jeshi la polisi la Kenya lawataka raia kuwa makini katika kipindi cha krismasi na mwaka mpya
Jeshi la polisi nchini Kenya, limetoa wito kwa wananchi wa taifa hilo kuwa makini kuhusu vitisho vya uwezekano wa kutokea kwa mashambulizi ya kigaidi kipindi cha krismasi na mwaka mpya.
Imechapishwa:
Akizungumza na televisheni binafsi K24, Inspekta Jenerali wa Polisi Hillary Mutyambai ametaka uangalifu mkubwa katika maeneo ya kuabudu lakini pia vituo vya usafiri wa umma.
Tahadhari hii imekuja, baada ya polisi nchini humo kuwakamata washukiwa wa Al Shabab kutoka nchini Somalia, baada ya kutekwa kwa wafanyakazi wanne wa kampuni ya ujenzi, Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.
Licha ya juhudi kubwa zilizopigwa katika kupambana na ugaidi nchini humo, jeshi la Polisi linasema, bado kuna tishio na kila mmoja anastahili kuwa makini wakati huu polisi wakiimarisha usalama katika maeneo ya umma nchini humo.
Kenya imeendelea kukabiliana na tishio la ugaidi tangu mwaka 2011, baada ya kutuma jeshi lake nchini Somalia kupambana na kundi la Al Shabab.