Askari wanane wa Burundi wauawa katika mapigano na waasi
Serikali ya Burundi imesema wanajeshi wake wanane wameuawa na wengine hawajulikani walipom Wilayani Mabayi, Mkoani Cibitoke, Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo baada ya kushambuliwa na watu wenye silaha.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Tangu kutokea kwa shambulizi hilo, mwishoni mwa wiki iliyopita, haijafahamika ni nani alihusika, na linakuwa shambulizi baya kuwahi kushuhudiwa tangu mwaka 2015.
Ripoti zinasema kuwa, shambulizi hilo lilitokea katika msitu wa Kibira, Kilomita karibu 10 kutoka mpaka wa Rwanda.
Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Wizara ya Ulinzi nchini humo Emmanuel Gahongano, amethibitisha kutokea kwa shambulizi hili ambalo liliwalenga zaidi ya wanajeshi 100.
Inaelezwa kuwa watu waliokuwa wamevalia mavazi ya kijeshi na yanayozuia kupenya kwa risasi, ndio waliohusika na shambulizi hilo.
Akizungumza na kupitia Televisheni ya taifa, Gahongano amesema wanashuku kuwa waliotekeleza shambulizi hili ni kundi la waasi kutoka Rwanda.
Hata hivyo, madai haya yamekanushwa vikali na Waziri wa Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki Olivier Nduhungirehe ambaye amesema, madai hayo hayana msingi wowote.