RSF yaomba kuachiliwa huru mara moja wanahabari 4 wanaoshikiliwa Burundi
Shirika la Kimataifa linalotetea wanahabari la Reporters Without Borders, linataka serikali ya Burundi, kuwaachilia huru wanahabari wanne wa Gazeti la Iwacu, waliokamatwa na maafisa wa usalama karibu na mpaka wa DRC mapema wiki hii.
Imechapishwa:
Wanahabari hao wanashikiliwa pamoja na derva wao katika eneo la Bubanza.
RSF inasema kuwa, inasikitisha kuwa wanahabari hao, walikuwa wanafanya kazi yao kama kawaida na hivyo wameendelea kuzuiliwa.
Waandishi hao wa habari wanne wa Gazeti binafsi la Iwacu nchini Burundi walikamatwa Jumanne mchana wiki hii walipokuwa katika kazi yao ya kutafuta habari katika mkoa wa Bubanza, Magharibi mwa nchi hiyo.
Waandishi hao wa habari waliokamatwa ni Christine Kamikazi, Agnès Ndirubusa, Térence Mpozenzi, Egide Harerimana na dereva wao Adolphe Masabarakiza.
Kulingana na taarifa iliyochapishwa kwenye ukurasa wa Twitter wa gazeti la Iwacu, viongozi wa mkoa wa Bubanza walipewa taarifa na waandishi hao kwamba watakuwa katika wilaya ya Musigati kwa kazi yao ya kila siku.