Kiongozi wa waasi Riek Machar akataa kujiunga katika serikali mpya Sudan Kusini
Kiongozi mkuu wa upinzani nchini Sudan Kusini Riek Machar amewaambia wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wanaozuru Juba, kuwa hatakuwa katika serikali ya pamoja na rais Salva Kiir inayotarajiwa kuundwa kufikia tarehe 12 mwezi Novemba.
Imechapishwa:
Machar amesema yeye na rais Kiir wameshindwa kukubaliana kuhusu namna ya kuliunganisha jeshi linaloomuunga mkono rais Kiir na vikosi vyake, akisema hataki kuiweka nchi yake kwenye mzozo kwa sababu suala hili muhimu halijapatiwa ufumbuzi.
Kushindwa kwa viongozi hawa wawili kuelewana kuhusu suala hili la usalama, kunatishia utekelezwaji wa mkataba wa amani nchini Sudani Kusini.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Machar alirejea jijini Juba kujadiliana na rais Kiir kuhusu suala hili lakini hawakuelewana.
Miezi kadhaa iliyopita, rais Kiir alitishia kuendelea na mpango wa kuunda serikali hiyo na wanasiasa wengine wa upinzani iwapo Machar hatakuwa tayari.