Pata taarifa kuu
RWANDA-USALAMA-SIASA

Benjamin Rutabana atoweka, RNC yanyooshewa kidole

Mwanamuziki kutoka Rwanda "Benja" Rutabana, mfuasi wa zamani wa chama tawala nchini Rwanda, RPF, ambaye aliachana na chama hicho na kujiunga na vuguvugu la upinzani lililo uhamishoni la RNC, hajulikani alipo, mwezi mmoja leo.

Benja Rutabana.
Benja Rutabana. © DR.
Matangazo ya kibiashara

Benjamin Rutabana, ambaye ni Mfaransa mwenye asili ya Rwanda alikuwa anaishi nchini Ubelgiji na familia yake.

Familia yake inasema ina wasiwasi baada ya taarifa za kutoweka kwake jijini Kampala, mji mkuu wa Uganda, Septemba 8.

Siku chache zilizopita, familia na marafiki wa Benjamin Rutabana waliandika barua wakiomba uongozi wa vuguvugu la RNC kuwajulisha alipo ndugu yao. Hata hivyo barua hiyo ilivuja kwenye mitandao ya kijamii.

Familia ya Rutabana inashuku kwamba vuguvugu la RNC lilihusika katika tukio hilo. Katika barua yao, waneleza kuwa Rutabana aliondoka Brussels jioni Septemba 4, na kuwawasili Kampala siku iliyofuata Tangu kuanza safari yake, Benjamin Rutabana alikuwa akizungumza kwa simu na mkewe Diane, kila siku hadi Septemba 8, tarehe ambapo mkewe alipokea simu yake ya mwisho.

"Sijui mume wangu yuko wapi, lakini ninachojua ni kuwa wanachama wa RNC wanajua mahali alipo, anaendeleaje, na kwamba sina mawasiliano naye."

Katika siku za kwanza, wanachama wa RNC walimueleza kuwa wanajua alipo mumewe. Benjamin Rutabana pia alionya juu ya mgawanyiko katika vuguvugu hili la RNC.

Kwa upande wake, katibu mkuu wa RNC Gervais Condo amefutilia mbali madai hayo na kubaini kwamba hawakujulishwa kuhusu safari yake nchini Uganda.

"Wakati ndugu yetu alisafari, hatukujulishwa kabisa. Sisi ni kundi ambalo linajumuisha watu wengi. Tunajaribu kujadili, kushawishi. Lakini kusema kwamba kuna mgawanyiko na malumbano ya ndani, hadi mtu kufanya safari yake binafsi, afuatiliwe, afanyiwe vibaya, tunasema hiyo haikubaliki. "

Gervais Condo amesema RNC inataka kushirikiana na familia ya Benjamin Rutabana kutoa mwanga kuhusu kutoweka kwake. Kwa upande wake, mkewe Rutabana ameendelea kuomba uchunguzi wa ndani ya RNC ufanyike ili kujua alipo mumewe. Pia amesema kwamba ameanza harakati za kukutana kwa mazungumzo na mamlaka nchini Ufaransa kwa sababu Benjamin Rutabana na mkewe wana uraia pacha.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.