Dengue yauwa wanne na wengine zaidi ya 4,000 wameambukizwa Tanzania
Serikali ya Tanzania inasema watu wanne wamepoteza maisha nchini humo kwa sababu ya homa ya Dengue na wengine 4,000 wameambukizwa na wanaendelea kupata matibabu.
Imechapishwa:
Waziri wa afya Ummy Mwalimu amewaambia wabunge jijini Dododma siku ya Ijumaa kuwa, watu watatu wamepoteza maisha jijini Dar es salaam na mwingine mmoja jijini Dodoma.
Aidha, ameeleza kuwa vifo vya watu wawili, vilitokea mwezi Mei.
"Ninaitaka Mikoa na Halmashauri zote nchini hasa zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Dengue na Malaria kusimamia kikamilifu kampeni za usafi wa mazingira na kuangamiza mbu. Pia natoa wito kwa wananchi kushirikiana na Serikali katika kuangamiza mbu wanaoeneza ugonjwa huu," alisema.
Serikali ya Tanzania ilitangaza kuwepo kwa homa hiyo ambayo haina dawa mwezi Machi mwaka 2019 , baada ya watu 11 kuambikizwa na kulazwa jijini Dar es salaam,
Waziri Mwalimu, ameongeza kuwa serikali imeweka mikakati ya kupambana na homa hiyo na kuagiza kuwa vipimo vya Dengue katika hospitali za umma, viwe bure.
Tayari vifaa vya kupima homa hiyo zaidi ya 30,000 vimetumwa katika hospitali mbalimbali nchini humo.