Uhusiano kati ya Tanzania na jumuiya ya kimataifa matatani
Serikali ya Tanzania imelaani kile ilichokiita "propaganda inayoendelea" baada ya Marekani kuwataka wananchi wake kuwa waangalifu nchini Tanzania. Hali ambayo inaonyesha sintofahamu katika utawala wa Rais Magufuli.
Imechapishwa:
"Yule aliyechapisha tahadhari hii hajui hata mahali inapatikana nchi yetu kwenye ramani". Hivi ndivyo serikali ya Tanzania ilivyojibu baada ya Marekani kutoa tahadhari hiyo mwishoni mwa wiki hii iliyopita.
Siku ya Jumatano, Marekani iliwataka wananchi wake kuwa makini ikiwa wataenda nchini Tanzania kwa sababu ya uhalifu na ukiukwaji wa haki za binadamu unaoendelea. Serikali ya Tanzania imesema hiyo ni "propaganda inayoendelea".
Hali hii inaonyesha kuzorota kwa uhusiano kati ya Tanzania na washirika wake.
Katika wiki za hivi karibuni, Umoja wa Ulaya ulimuitisha nyumbani balozi wake na kuahidi kupunguza msaada wake wa kifedha; huku Benki ya Dunia na Denmark wakisitisha mipango kadhaa ya maendeleo kwa Tanzania.
Wataalamu pia wana wasiwasi kuhusu kuzorota kwa uchumi katika siku zijazo. Ukuaji wa uchumi unasimamia kwenye 7%. "Unaweza kwenda chini ya 3%," mwanadiplomasia mmoja ameonya. "Nchi ya Tanzania inakabiliwa na mdororo wa kiuchumi.
Mtaalam mwingine ameshtumu kuhusu kuwekwa hatarini kwa mikataba na washirika wa kigeni, mashambulizi dhidi ya wajasiria mali wa ndani, hususan wafanyabiashara kutoka India, kupungua kwa uwekezaji katika sekta muhimu au ukaguzi na marekebisho mbalimbali.
"Uchumi umejifungia ndani yake. Hatari ni kwamba wawekezaji kutoka nje watosita kuingiza mali zao nchini. Zote hizo ni ishara mbaya zinazoonyesha kushuka kwa uchumi, "mtaalam mwengine ameonya.