Gavana aliyeshtakiwa nchini Kenya kwa mauaji ya mpenzi wake, apewa dhamana
Mahakama Kuu jijini Nairobi nchini Kenya, imemwachilia kwa dhamana ya Dola 50,000 Gavana wa Kaunti ya Migori Okoth Obado anayetuhumiwa kumuua mpenzi wake aliyekuwa mja mzito Sharon Otieno.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Jaji Jessie Lessit, ametoa uamuzi huo na kumtaka Gavana Obado, kuwasilisha hati yake ya kusafiri lakini pia kumwonya dhidi ya kuwasiliana na familia ya Sharon.
Aidha, ametakuwa kutosafiri zaidi ya Kilomita 20, akiwa katika Kaunti ya Migori, kutozungumzia suala hili katika mikutano ya kisiasa na kuripoti kila mwezi katika Ofisi ya Naibu msajili wa Mahakama.
Mahakama imeonya kuwa, iwapo masharti hayo yatavunjwa, dhamana hiyo itafutwa.
Gavana huyo aliyekamatwa mwezi Septemba, amekuwa akizuiwa katika Gereza la Industrial Area jijini Nairobi kwa siku 33, baada ya kunyimwa dhamana.
Hata hivyo, Mahakama hiyo imekataa kuwapa dhamana washukiwa wengine wawili Michael Oyamo na Caspal Obiero kwa hofu kuwa wanaweza kuharibu ushahidi.
Kesi dhidi ya Gavana Obado na washtakiwa wenzake wawili waliokanusha madai ya kuhusika na kifo cha Sharon, inatarajiwa kuanza tarehe 17 mwezi Mei mwaka 2019.
Sharon Otieno alizikwa wiki iliyopita huku wanaharakati wakitaka waliohusika wachukuliwe hatua kali.