Kangi Lugola:Tunaendelea kumsaka Mohammed Dewji
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania amesema serikali ya nchi hiyo inaendelea kumsaka mfanyabiashara mashuhuri Mohammed Dewji na kuonya wananchi kutotumia mitandao ya kijamii kujenga hofu.
Imechapishwa:
Hii ni mara ya kwanza kwa Lugola kujitokeza hadharani kuzungumzia kadhia ya kutekwa nyara kwa Dewji ambaye sasa imetimia zaidi ya saa 28 tangu ilipoarifiwa kuwa ametekwa nyara.
Lugola amesema kufikia sasa watu 20 wanashikiliwa na polisi kufuatia kisa cha kutoweka kwa Mo ili kulisaidia jeshi la polisi katika upepelezi.
"Asitokee mtu yeyote anayetaka kutumia matukio haya kama mtaji wa kisiasa au wa kujitafutia umaarufu na kuonesha nchi nyingine zinazotaka kuwekeza au zinawekeza kwamba nchini hakuna amani na usalama,'ameonya Waziri huyo, ambaye amejizolea umaarufu kwa kutoa maagizo mengi kwa watendaji wake.
Kuhusu matukio ya nyuma ya utekaji Lugola, amesema polisi bado inaendelea na uchunguzi kwa kuwa uhai wa kila mtanzania una thamani na kwamba rais John Magufuli aliapa kulinda raia na mali zao.
Katika hatua nyingine Lugola ameambia wanahabari kuwa watu 75 wametekwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Baadhi ya matukio hayo ni kutekwa kwa mwanahabari Azory Gwanda na Ben Saanane, aliyekuwa msaidizi wa kiongozi wa upinzani nchini humo, Freeman Mbowe.