Watu 31 wafariki dunia kufuatia maporomoko ya ardhi Uganda
Watu Thelathini na mmoja wamefariki dunia katika maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa wilayani Bududa, mashariki mwa Uganda, wakuu wa serikali katika wilaya hiyo wamesema.
Imechapishwa:
Maafisa wanataja kuwa ni maporomoko makubwa na hatari kuwahi kushuhudiwa nchini Uganda.
Msemaji wa shirika la msalaba mwekundu nchini Uganda Irene Nakasita amesema maji yaliendelea kuongezeka wakati ikinyesha mvua hiyo kubwa, huku akaongeza kuwa huenda idadi ya vifo ikaongezeka.
Taarifa fupi ya Irene Nakasita, imesema kuwa kuna hali ya wasiwasi mkubwa katika wilaya nzima ya Bududa, wakati huu wa mvua.
Kamishna wa kamati inayozuia majanga asilia mjini Bukalasi, katika Wilaya ya Bududa Martin Owor amekaririwa na shirika la habari la Ufaransa AFP kuwa hadi sasa miili ya watu Kumi na mmoja imepatikana wakati huu shughuli za uokoaji zikiendelea.
Kwa mujibu wa wakazi wa wilaya ya Bududa, kata ndogo ya Bukalasi, yenye milima mingi, maporomoko ya matope yalianza kushuhudiwa saa nane alasiri, wakati maji, matope, na miti ikiporomoka kutoka juu ya mlima, kufunika makao ya watu hadi sehemu tambarare madukani.