Kenya: Tarehe 10 Oktoba ni siku ya mapumziko
Serikali ya Kenya imetangaza kuwa kesho, itakuwa ni siku ya mapumziko ya kitaifa baada ya Mahakama kuagiza kuwa, sikikukuu ya Moi, kumkumbuka rais wa zamani Daniel Torotich Arap Moi irejeshwe tena.
Imechapishwa:
Hata hivyo, Mahakama imesema Moi Day sio sikukuu ya taifa lakini inasalia kuwa siku ya mapumziko, huku serikali kupitia Waziri wa Mambo ya ndani Fred Matiang'i akiwaambia Wakenya kuwa serikali haiwezi kuwachagulia namna ya kuadhimisha siku hiyo.
Matiang’i ametangaza haya kufuatia uamuzi wa jaji wa mahakama kuu George Odunga uliotolewa baada ya miaka saba ya kutoadhimishwa kwa sikukuu ya Moi Day.
Rais Mstaafu Moi amekuwa akitumia siku hiyo, kuwatembelea wasiojiweza na kutoa misaada.
Jaji Odunga katika uamuzi wake Novemba 2017 alisema kutoadhimishwa kwa tarehe 10 Oktoba iliyofahamika kama moi day awali kunakiuka sheria ya sikukuu za kitaifa.
Sikukuu ya Moi Day haijaadhimishwa tangu kupitishwa kwa katiba mpya 2010.