Mwanamuziki na Mbunge Bobi Wine aachiliwa huru kwa dhamana Uganda
Mwanamuziki maarufu na Mbunge Bobi Wine, ambaye alishtakiwa kwa kosa la uhaini nchini Uganda, amechiliwa huru kwa dhamana Jumatatu wiki hii. Uamuzi huu umechukuliwa na mahakama ya kaskazini mwa nchi baada ya kuwekwa rumande kwa muda wa wiki huko Gulu.
Imechapishwa:
Robert Kyagulanyi anayejulikana kwa jina la Bobi Wine, alikamatwa pamoja na watuhumiwa wengine 33 kufuatia tukio la Arua, kaskazini mwa Uganda. Anashtumiwa kuhusika katika vurugu za kurushia mawe magari ya msafara wa rais Yoweri Kaguta Museveni wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa eneo bunge la Arua.
Leo Jumatatu, Jaji Stephen Mubiru, Mkuu wa mahakama ya Gulu (kaskazini), alikubali ombi la Kyagulanyi na baadhi ya watuhumiwa wenzake, ikiwa ni pamoja na wabunge wawili wa upinzani kuachiliwa huru kwa dhamana.
Kyagulanyi, mwenye umri wa miaka 36, ameibuka kama msemaji wa vijana wa Uganda na mpinzani mkuu wa rais Yoweri Museveni tangu uchaguzi wake kama mbunge mnamo mwaka 2017. Kufungwa kwake kulizua maandamano makubwa katika maeneo mbalimbali nchini Uganda, ikiwa ni pamoja na mji mkuu, Kampala, ambapo polisi ilitumia nguvu kupita kiasi kwa kuzima maandamano hayo.