Pata taarifa kuu
KENYA-MAREKANI-TRUMP-KENYATTA

Rais Kenyatta kuwa kiongozi wa tatu kutoka Afrika kukutana na Trump

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta anatarajiwa kukutana na rais wa Marekani Donald Trump Agosti 27 katika Ikulu ya White House, jijini Washington DC.

Rais wa Kenya  Uhuru Kenyatta akiwa amezingizwa na wakuu wa jeshi la usalama nchini humo jijini Nairobi mwaka 2017
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta akiwa amezingizwa na wakuu wa jeshi la usalama nchini humo jijini Nairobi mwaka 2017 REUTERS/Thomas Mukoya
Matangazo ya kibiashara

Rais Kenyatta atakuwa kiongozi wa tatu wa bara Afrika, kukutana na rais Trump baada ya Muhamadu Buhari wa Nigeria na Abdel Fattah al-Sisi wa Misri.

Ikulu ya Marekani imesema, Kenya ni nchi muhimu barani Afrika na rais Trump na Kenyatta watajadili masuala yenye umuhimu kati ya nchi hizo mbili ikiwa ni pamoja na usalama na biashara.

Tangu alipoingia madarakani mwaka 2013, rais Kenyatta amekuwa katika harakati za kuimarisha uhusiano wa nchi ya Kenya na Marekani kama taifa muhimu na mshirika wake wa karibu barani Afrika.

Mkutano wa Kenyatta na Trump, unatuma ujumbe kuwa Kenya linasalia taifa muhimu barani Afrika na Afrika Mashariki kutokana na harakati zake za kusaidia kurejea kwa amani nchini Sudan Kusini na Somalia.

Kenya imekuwa katika mstari wa mbele kuwaleta katika meza ya mazungumzo rais Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar.

Kenyatta alikuwa jijini Khartoum Jumapili iliyopita, kushuhudia utiwaji sahihi wa mkataba wa amani kati ya viongozi hao wawili.

Aidha, Kenya ni imetoa nafasi kwa maelfu ya wakimbizi kutoka Somalia, Sudan Kusini, Burundi na DRC kutokana na mizozo katika nchi zao.

Wachambuzi wanasema rais Kenyatta anatarajiwa kutumia mkutano wake na Trump kujadili pia ajenda zake nne, chakula, makaazi, afya na uzalishaji kuona namna Marekani inavyoweza kuisaidia serikali yake ili kutekeleza malengo hayo kabla ya kuondoka madarakani mwaka 2022.

Ziara hii inakuja baada ya rais Kenyatta kuwa kiongozi wa kwanza wa nchi hiyo, kuwahotubia viongozi wa mataifa saba makubwa kiuchumi G7 nchini Italia mwaka 2017 na kuwahimiza viongozi wa dunia kupambana na umasikini, mabadiliko ya hali ya hewa, uhamiaji haramu na ugaidi.

 

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.