Kampuni ya CRBC yakabiliwa na tuhuma za ubaguzi Kenya
Wafanyakazi wa Shirika la Reli nchini Kenya, wanaofanya kazi katika mradi wa reli ya Kati kutoka mjini Mombasa hadi Nairobi, wanalalamikia ubaguzi kutoka kwa wakuu wa kampuni ya China Road and Bridge Corporation (CRBC) inayosimamia mradi huo kwa muda wa miaka 10.
Imechapishwa:
John Chumo, Katibu Mkuu wa chama cha Wafanyakazi hao RAWU, amekiambia kituo kimoja cha habari nchini humo kuwa amekuwa akipokea malalamishi ya wafanyakazi wazawa kunyanyaswa kwa sababu ya rangi yao.
Aidha, amesema madereva wa treni hiyo ya mwendo kasi ambao ni raia wa nchi hiyo wanalipwa Dola 300 kwa mwezi huku wale wa China ambao wanafanya kazi sawa na wamefuzu kwa kiwango sawa, wakilipwa Dola 1,000.
“Ubaguzi huu wa malipo haikubaliki, kwa sababu kazi inayofanywa ni moja,” amesema Chumo.
Kutokana na tuhma hizi, Shirika la Reli nchini Kenya, limesema linaanzisha uchunguzi binafsi na kutoa saa 72 kwa viongozi wa kampuni hiyo ya China kujibu madai hayo.