Pata taarifa kuu
UHURU WA HABARI-MAFUGULI-TANZANIA

Jamii Forums wafunga mtandao wao Tanzania

Mtandao mashuhuri wa Jamii Forums umefunga huduma zake nchini Tanzania kutokana na notisi iliyotolewa na mamlaka ya mawasiliano Tanzania (TCRA).

Nembo ya mtandao wa Jamii Forum ambao umefungwa Tanzania
Nembo ya mtandao wa Jamii Forum ambao umefungwa Tanzania Screenshot/Youtube
Matangazo ya kibiashara

Jamii Forums ni jukwaa maarufu zaidi nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla linalotoa huduma zake kwa njia ya mtandao na inaaathirika kutokana na kuanza kutekelezwa kwa kanuni zinazosimamia maudhui ya kwenye mtandao.

Juni 10, Mamlaka ya mawasiliano Tanzania ilitoa notisi ikieleza kuwa ni kosa kisheria kutoa na kuchapisha taarifa kwa njia ya mitandao bila kuwa na leseni.

Tangazo hilo limeainisha kuwa mwisho wa kupata leseni ni Juni 15 mwaka huu na baada ya hapo uchapishaji wa taarifa kwenye blog, majukwaa ya mtandaoni, radio na televisheni za mtandao itakuwa ni kukiuka sheria.

Aidha kwa watakaobainika kuchapisha habari bila kuwa na leseni watachukuliwa hatua za kisheria.

Kutokana na tangazo hili la TCRA, wamiliki wa mtandao wa Jamii Forums wametoa taarifa kwa watumiaji wake kueleza kuwa hawatapatikana tena nchini Tanzania hadi pale changamoto zilizopo zitakaposhughulikiwa.

Taarifa ya Jamii Forum imesema “Kutokana na notisi iliyotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania inayotoa muda mfupi wa kututaka kusitisha utoaji wa huduma baada ya Juni 11, 2018 tunalazimika kutii mamlaaka na hivyo huduma hii haitapatikana kwa muda wakati tukifanya taratibu za kuhakikisha huduma zinarejea,”

Hata hivyo, baadhi ya wachangiaji wa mtandao huo wamesema hatua hiyo imelenga mahsusi kudhibiti uchapishaji wa habari kwa njia ya mtandao.

“Kwa vile hii ni mbinu ya kudhibiti Jamii Forums ituachie angaalau tusome maudhui ya zamani,”amechangia mwanahabari mkongwe nchini Tanzania Pascal Mayalla.

Mtandao mwingine ulioathirika na amri ya mamlaka ya mawasiliano Tanzania ni habari24 ambao pia umekuwa ukichapisha habari za siasa, michezo na burudani.

Mkurugenzi wake Exaud Mtei ameiambia RFI kuwa ameshindwa kupata fedha ili kukamilisha usajili.

Kanuni za maudhui ya mtaandaoni zimepingwa mara kadhaa na wadau wa tasnia ya habari ikiwemo Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ambao hivi karibuni walifungua kesi mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Mtwara ili kuweka zuio la muda lakini hata hivyo mahakama ilitupilia mbali kesi hiyo na kuagiza kuanza kutumika kwa kanuni hizo.

Katibu Mkuu wa Jukwaa la Wahariri nchini Tanzania, Neville Meena hivi karibu aliiarifu RFI Kiswahili kuwa utekelezaji wa kanuni mpya za maudhui ya mtandaoni, utaua upashaji habari kwa umma.

Hata hivyo, Waziri wa Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo Dr Harrison Mwakyembe, mara kadhaa ametetea uamuzi wa kutungwa kwa kanuni mpya akisema zinalenga kulindaa maadili katika sekta ya habari.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.