Rais Nkurunziza atangazwa kuwa kiongozi wa maisha wa chama cha CNDD-FDD
Chama tawala nchini Burundi cha CNDD-FDD kimemtangaza rais Pierre Nkurunziza kuwa kiongozi wa juu kabisa wa chama hicho, hatua inayomfanya awe kiongozi wa maisha.
Imechapishwa:
Licha ya taarifa ya chama hicho iliyotolewa mwishoni mwa juma kutoeleza kwa kina kuhusu nafasi mpya waliyompa Nkurunziza, lakini ni wazi sasa kiongozi huyo anafanywa kuwa mtawala wa maisha, hatua inayozidisha sintofahamu zaidi kwenye siasa za nchi hiyo.
Haijafahamika ikiwa kutakuwa na marekebisho mengine ya katiba tofauti na yale yanayotarajiwa kupigiwa kura mwezi Mei mwaka huu ambapo ikiwa yataidhinishwa yatamruhusu kuwania urais kwenye uchaguzi wa mwaka 2020 na kumfanya abaki madarakani hadi mwaka 2034.
Hali ya kisiasa nchini Burundi imekuwa mashakani tangu mwaka 2015, wakati kiongozi huyo alipoamua kuwania urais kwa muhula wa tatu kinyume cha mkataba wa amani wa Arusha.
Wapinzani wake walijitokeza kuandamana, hatua ambayo iliikasirisha serikali ya Bujumbura ambayo ilitumia nguvu dhidi ya waandamanaji na kusababisha mamia ya watu kupoteza maisha na maelfu kuyakimbia makwao.