Wafuasi wa upinzani nchini Kenya wataka Balozi wa Marekani kuondolewa
Wafuasi wa muungano wa upinzani nchini Kenya NASA, siku ya Ijumaa waliandamana mbele ya Ubalozi wa Marekani jijini Nairobi, kutaka kuondoka nchini humo Balozi wa Marekani Robert Godec.
Imechapishwa:
Maandamano haya, yanakuja wiki moja baada ya Godec na Mabalozi wengine wa mataifa ya Magharibi kumtaka kiongozi wa NASA Raila Odinga kumtambua Uhuru Kenyatta kama rais halali wa nchi hiyo.
Wafuasi wa NASA, wamemtaka Balozi huyo kuacha kuingilia siasa za nchi hiyo, wakimtaka rais wa Marekani Donald Trump kumrudisha nyumbani Godec.
Wakiwa wamebeba mabango wakiimba nyimbo za kumsifia kiongozi wao, waandamanaji hao walimtaka Balozi Godec kumheshimu Odinga na kumtambua kama kiongozi wao.
Odinga akiwajibu Mabalozi hao, aliwaambia kuwa Kenya sio nchi ya kutawaliwa na inaweza kutatua changamoto zake bila ya kuingiliwa na mataifa ya nje.
Mabalozi wa mataifa ya Magharibi, wamekosoa hatua ya Odinga kujiapisha mwezi Januari kama rais wa wananchii.
Odinga ameapa kutomtambua Uhuru Kenyatta kama rais wa nchi hiyo.