Mahakama ya Juu nchini Kenya yashindwa kuendelea na kesi ya kuzuia Uchaguzi wa urais
Mahakama ya Juu nchini Kenya, imesema haiwezi kusikiliza shauri la wapiga kura watatu waliokwenda katika Mahakama hiyo kutaka Uchaguzi uliopangwa kufanyika siku ya Alhamisi kuahirishwa.
Imechapishwa:
Jaji Mkuu David Maraga amesema ni vigumu kwa kesi hiyo kuendelea kwa sababu wamesalia Majaji wawili ambao hawawezi kuendelea na kesi hiyo.
“Tunaomba radhi kwa changamoto hii iliyojitokeza, na kwa namna hali ilivyo, hatuwezi kuendelea na kesi hii,” alisema Jaji Maraga.
Maraga ameeleza kuwa Naibu wake Philomena Mwilu ambaye mlinzi na dereva wake alipigwa risasi na watu wasiojulikana hawezi kufika Mahakamani.
“Nimesalia na Jaji Isaac Lenaola, na kwa mujibu wa sheria iliyounda Mahakama ya Juu, itakuwa vigumu kuendelea kwa kesi hii,” aliongeza Maraga.
Mawakili wa Tume ya Uchaguzi wanasema kwa kesi hiyo kushindwa kuendelea, Tume itaendelea na maandalizi ya Uchaguzi hapo kesho.
Naye Wakili wa wapiga kura hao Harun Ndubi, amesema ameshangazwa na hatua hiyo na kusema kutofika kwa Majaji hao kazini ni kinyume cha Katiba.
“Ni siku ya huzuni nchini Kenya, na Tume ya Uchaguzi ikijaribu kuendelea na Uchaguzi huo usiokubalika, itakuwa kinyume cha sheria,” alisema Orengo.
Katika hatua nyingine, Mahakama Kuu imesema maafisa wa kusimamia Uchaguzi katika maeneo bunge yote 290 haukufanyika kwa mujibu wa sheria.