Wasifu: Mfahamu zaidi rais Uhuru Kenyatta
Uhuru Muigai Kenyatta alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa rais wa nchi hiyo mwaka 2013, baada ya uchaguzi uliokuwa na ushindani mkali kati yake na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, kama ilivyokuwa mwaka huu.
Imechapishwa:
Odinga alikwenda Mahakamani kupinga ushindi wa Kenytta, kwa madai kuwa kulikuwa na wizi wa kura lakini Mahakama ya Juu ikashikilia uamuzi kuwa Kenyatta alishinda.
Rais Kenyatta mwenye umri wa miaka 55, ni mtoto wa rais wa kwanza wa nchi hiyo Jomo Kenyatta, aliyeongoza Kenya baada ya kupata uhuru mwaka 1963.
Kenyatta aliingia kwenye uwanja wa kisiasa mwaka wa 1997 baada ya kuhimizwa kufanya hivyo na rais mstaafu Daniel Torotich Arap Moi.
Mwaka 2002, wakati Moi alipostaafu siasa, alimteua Kenyatta kuwa mgombea urais na kumrithi kupitia chama cha KANU, lakini alishindwa na mgombea wa wakati huo wa upinzani Mwai Kibaki kupitia muungano wa kisiasa wa NARC.
Kushindwa kwake, kulitikisa chama cha KANU ambacho hadi sasa kimekosa umaarufu pamoja na kwamba bado kipo katika siasa za nchi hiyo.
Baada ya Uchaguzi uliojawa na utata wa mwaka 2007, Uhuru Kenyatta alikuwa miongoni mwa watu sita walioshtakiwa katika Mahakama ya Kimataifa ya ICC mjini Hague kwa madai ya kuchochea machafuko ya baada ya Uchaguzi uliosababisha zaidi ya watu 1,000 kupoteza maisha.
Hata hivyo, mwaka 2015 mashtaka dhidi yake yaliondolewa kwa ukosefu wa ushahidi.