Kipindupindu chazuka jijini Nairobi, 30 walazwa
Serikali ya Kaunti ya Nairobi nchini Kenya imeanza operesheni ya kufunga vituo vya kuuza vyakula ambavyo havina leseni hasa vibanda vinavyopatikana pembezoni mwa barabara.
Imechapishwa:
Hatua hii inakuja baada ya watu thelathini wakiwemo Mawaziri wawili kulazwa hospitalini baada ya kubainika kuwa na dalili ya kipindupindu.
Waziri wa afya katika kaunti hiyo Daktari Bernard Muia amesema vituo visivyokuwa na leseni vitafungwa katika jithada za kukabiliana na ugonjwa huu hatari.
Aidha, Daktari Muia amewataka wafanyibiashara katika jiji hilo kuwa waangalifu kuhusu chakula wanachowaandaliwa wateja wao na kudumisha usafi wa hali ya juu ili kuepusha maambukizi.
“Ikiwa utabaini kuwa una dalili za kuumwa tumbo, kutapika, tafadhali hakikisha kuwa unakwenda hospitalini haraka iwezekanavyo,” amesema Daktari Muia.
Watalaam wanasema kuwa, uhaba wa maji jijini Nairobi ni chanzo cha maambukizi haya ambayo hata hivyo Wizara ya afya nchini humo inasema inadhibiti.