Rais Salva Kiir aagiza kubadilishwa jina la jeshi la Sudan Kusini
Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir ametoa agizo la kubadilisha jina la jeshi la nchi hiyo kutoka SPLA na sasa litafahamika kuwa SSDF.
Imechapishwa:
SSDF maana yake ni jeshi la ulinzi la Sudan Kusini.
Aidha, rais Kiir amemrejesha Meja Jenerali Dau Aturjong Nyuo katika jeshi la nchi hiyo.
Mwaka 2014 Aturjong alijiondoa katika jeshi la nchi hiyo na kuungana na vikosi vya upinzani vya SPLM-IO vinavyoongozwa na Riek Machar, baada ya kuzuka kwa makabiliano jijini Juba.
Katika hatua nyingine, rais Kiir ameagiza kubadilishwa kwa muundo wa uongozi wa jeshi nchini humo.
Sasa kutakuwa na Mkuu wa Majeshi, Waziri wa Ulinzi, na Mkuu atakayeshughulikia maslahi ya wanajeshi waastafu na waliohusika pakubwa katika vita vya kuikomboa nchi hiyo.
Kanuni za kijeshi nchini humo, zinampa uwezo na mamlaka rais kubadilisha muundona mfumo wa jeshi kama amiri jeshi Mkuu wa majeshi nchini humo.