Marekani kutoa mafunzo kwa wanajeshi wanaopambana na Al Shabab
Marekani imesema inatuma jeshi lake nchini Somalia kwenda kutoa mafunzo kwa wanajeshi wanaopambana na kundi la kigaidi la Al Shabab.
Imechapishwa:
Itakuwa ni mara ya kwanza kwa Marekani kurejesha jeshi lake nchini humo baada ya kuliondoa mwaka 1994.
Mwaka 1993, wanajeshi 18 wa Marekani waliuawa nchini Somalia baada ya ndege zao mbili kuangushwa mjini Mogadishu hali ambayo iliwashangaza wanajeshi wa Marekani na dunia.
Mwezi uliopita, rais Donald Trump alisema serikali yake itakabiliana vikali na magaidi wa Al Shabab ambao wanaendelea kutishia usalama wa Afrika Mashariki.
Hata hivyo, Marekani imekuwa ikituma silaha, fedha lakini pia watalaam wake wa maswala ya usalama kushirikiana na wanajeshi wa Umoja wa Afrika AMISOM kukabiliana na wanamgambo hao.
Al Shabab imeendelea kuwa tishio kwa usalama wa mataifa ya Afrika Mashariki.