Rais Kenyatta aagiza kulipwa kwa Madaktari waliogoma kwa siku 100
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta ameagiza kulipwa kwa Madaktari waliogoma kwa siku 100 wakishinikiza nyongeza ya mshahara na kuboreshwa kwa mazingira ya kufanya kazi.
Imechapishwa:
Agizo hili limekuja baada ya Baraza la Magavana nchini humo linaloshughulikia sekta ya afya kusema kuwa haliwezi kuwalipa mshahara Madaktari hao.
Chama cha Madaktari nchini humo uliokuwa umeapa kuitisha mgomo mpya kuanzia siku ya Alhamisi ikiwa Magavana wangeendelea na msimamo wao wa kutowalipa.
"Naomba kwa heshima Magavana wawalipe Madaktari,” alisema.
Pamoja na hilo, rais Kenyatta amesema ikiwa Madaktari hao watagoma tena, watafutwa kazi.
“Naapa kuwa wakigoma tena, tutawafuta kazi,” aliongezea.
Aidha, amesema kuwa alikasirishwa sana na mwenendo wa Madaktari hao wakati wa mgomo na kueleza kuwa haikuwa mapenzi ya serikali wagonjwa kupoteza maisha kwa kukosa huduma za afya.
“Tunaweza kuwafufua waliofariki dunia wakati wa mgomo kwa sababu Madaktari hawakuwa kazini,” aliuliza rais Kenyatta kwa hasira.
Serikali ya Kenya imeamua kuwaajiri Madaktari 500 kutoka nchini Tanzania, baada ya mgomo huo, mchakato ambao umesitishwa kwa muda baada ya Madaktari kadhaa kwenda Mahakamani.
Madaktari hao wanataka serikali ya Kenya kuwaajiri Madaktari zaidi ya 1000 ambao hawana kazi kabla kuwaajiri wengine kutoka nje ya nchi.