Uganda na Tanzania zakubaliana kuimarisha mahusiano ya kibiashara
Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli na mwenzake wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni, wamekubaliana kuimarisha biashara kati ya nchi hizo mbili, ambapo wamesema takwimu zinaonesha nchi hizo zinabadilishana vitu kwa wingi zaidi ukilinganisha na mataifa mengine.
Imechapishwa:
Akizungumza ikulu ya jijini dar es Salaam, wakati wa ziara ya rais wa Uganda, rais wa Tanzania John Magufuli, amesema viongozi hao wamekubaliana kushirikiana kibiashara na kuimarisha zaidi uhusiano wao hasa wakati huu wanapotaka kuwa nchi za viwanda.
Kwa upande wake rais Museveni, alitumia sehemu ya Hotuba yake kukumbusha historia ya uhusiano wa Tanzania na Uganda, akisema ni Tanzania pekee kwa nchi za Afrika, ndiyo iliyosimama na Uganda kumuondoa nduli Iddi Amini, hivyo nchi yake inaithamini sana Tanzania na ndio maana akaamua kuitembelea.
Viongozi hawa pia wamekubaliana kushirikiana katika kuhakikisha bomba la mafuta kati ya Tanzania na Uganda linajengwa haraka na kwa wakati ili kuanza kusafirisha mafuta ghafi kutoka nchini Uganda, bomba ambalo awali lilikuwa lijengwe kati ya Uganda na Kenya.
Pia wamezungumzia masuala ya ushirikiano wa kiusalama, na hasa kuhakikisha kuwa nchi wanachama zinakuwa na amani na utulivu pamoja na kushughulikia kikamilifu mzozo wa nchi jirani ya Burundi.
Hii leo rais Museveni anatarajiwa kutembelea viwanda vya Azam kama sehemu ya Ziara yake ambayo anatarajia kuitamatisha jioni ya leo.