Bunge nchini Kenya labadilisha sheria ya Uchaguzi, upinzani wakimbilia Mahakamani
Wabunge wa serikali nchini Kenya, limeifanyia marekebisho sheria ya Uchaguzi, kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2017.
Imechapishwa:
Mabadiliko hayo yataiwezesha Tume ya Uchaguzi kutumia njia ya kawaida kuwatambua wapiga kura na kuwasilisha matokeo ya urais ikiwa mfumo wa teknolojia hautawezekana.
Ni mabadiliko ambayo yamepingwa vikali na wabunge wa upinzani ambao waliondoka bungeni wakati wa mjadala wa kuirekebisha sheria hiyo baada ya kudai kuwa wabunge wa serikali walikuwa wamejihami kwa silaha hatari na walilenga kuwadhuru.
Aidha, upinzani unadai kuwa serikali ya rais Uhuru Kenyatta imebadilisha sheria hiyo ili kutengeneza mazingira ya kuiba kura, madai ambayo serikali inakanusha.
Wabunge wa serikali wanasema, mabadiliko hayo yataipa nafasi Tume ya Uchaguzi kutumia mfumo mbadala ikiwa mtandao utasumbua siku ya kupiga kura mwezi Agosti mwaka ujao.
Baada ya marekebisho hayo kupitishwa, Mahakama imesema haiwezi kuzuia kikao cha bunge kuendelea kwa sababu mabadiliko hayo bado hayajawa sheria.
Upinzani umesema utahakikisha kuwa Uchaguzi wa mwaka ujao haufanyiki baada ya kufanyika kwa mabadiliko hayo na hata kutishia kuwepo kwa maandamano.