Hakimu amtembelea Besigye Gerezani
Hakimu wa Mahakama ya Nakawa jijini Kampala nchini Uganda James Ereemye amemtembelea kiongozi wa chama cha upinzani FDC Kizza Besigye anayezuiliwa katika Gereza la Luzira kwa tuhma ya kosa la uhaini.
Imechapishwa:
Hakimu huyo amesema alimtembelea Besigye mwishoni mwa mwezi uliopita, baada ya Besigye kudai kuwa haki zake zinakeukwa ndani ya Gereza hilo.
Ereemye amesema alikwenda kujionea mwenye namna mambo yalivyo anakozuiliwa Besigye tangu mwezi Mei mwaka huu, lakini hakueleza mengi kuhusu alichokiona.
Upinzani nchini Uganda umekuwa ukishinikiza kuachiliwa huru kwa Besigye baada ya kukamatwa kwa kujiapisha kuwa rais wa nchi hiyo mapema mwezi Mei siku moja kabla ya kuapishwa kwa rais Yoweri Museveni ambaye ameongoza nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 30.
Besigye ameendelea kudai kuwa alishinda uchaguzi wa mwezi Februari mwaka huu, na kuishtumu Tume ya Uchaguzi kwa kumwibia kura rais Museveni.
Kesi nyingine ya kutotii amri ya maafisa wa polisi wakati wa kampeni ya uchaguzi Mkuu mwezi uliopita, iliondolewa na serikali bila ya kutoa sababu zozote.