Trump, Kim Jong-Un wawasili Singapore kwa mkutano wa kihistoria
Rais wa marekani Donald Trump na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-Un wamewasili Singapore kuhudhuria mkutano wa kihistoria unaolenga kumaliza sintfahamu katika rasi ya Korea.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kim aliwasili katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Changi kwa ndege ya China 747 , gazeti la kila siku la Singapore, Straits Times limearifu.
Aidha tovuti ya The Flightradar24 imepasha kuwa hakukuwa na ndege nyingine yoyote ya abiria angani, wakati kiongozi Kim akiwasili uwanjani hapo.
Rais wa Marekani Trump, aliwasili katika Uwanja wa ndege wa kijeshi wa Paya Lebar saa 2:21 kwa saa za Singapore sawa na saa 9:21 kwa saa za Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya nje ya Singapore ni kwamba Kiongozi wa Korea Kaskazini anatazamiwa kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Singapore Lee Hsien Loong.
Aidha inatazamiwa, wanadiplomasia kutoka mataifa mawili na wale wa Singapore watakutana kesho, kabla ya mkutano wa Jumanne.
Mkutano baina ya Kim na Trump utafanyika Jumanne ya Juni 12, lakini tayari umekuwa mjadala mpana katika vyombo vya habari duniani na mara kadhaa rais Trump amesisitiza mazungumzo baina ya Washington na Pyongyang yatakuwa mwanzo wa kurejesha uhusiano baina ya Pyongyang na jumuiya ya kimataifa.