Dennis Kimetto avunja rekodi ya dunia mwaka 2014
Katika mchezo wa Riadha, kitakachokumbukwa mwaka huu ni kuvunjwa kwa Rekodi ya dunia katika mbio za Marathon iliyovunjwa na Mkenya Dennis Kimetto wakati wa mashindano ya Berlin Marathon nchini Ujerumani tarehe 28 mwezi wa Septemba.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kimetto mwenye umri wa miaka 30, alivunja rekodi hiyo ya dunia kwa kumaliza mbio hizo kwa muda wa saa 2 dakika 2 na sekunde 57 na kuwa mwanaridha wa kwanza kuwahi kukimbia mbio za Marathon chini ya saa mbili na dakika 3.
Vile vile katika mchezo wa Riadha, itakumbukwa kesi ya mwanariadha mlemavu kutoka Afrika Kusini Oscar Pistorius, ambaye alihukumiwa kifungo cha miaka mitano baada ya kupatikana na kosa la kumuua bila kukusudia mpenzi wake Reeva Steenkamp.
Hata hivyo kesi ya mwanariadha huyo wa zamani ilirejeshwa Mahakamani kufuatia ombi la Ofisi ya mwendesha mashitaka.
Desemba 10 mwaka 2014, jaji aliruhusu kesi hiyo isikilizwe katika kitengo cha rufaa, baada ya viongozi wa Mashitaka kukata rufaa kwa hukumu aliyopewa Oscar Pistorius.
Baada ya miezi minane kesi yake ikisikilizwa, Oscar Pistorius alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kwa kosa la kumuua bila kukusudia mpenzi wake Reeva Steenkamp mwezi Februari mwaka 2013. Hukumu ambayo Ofisi ya Mashitaka haikukubaliana nayo.
Majaji walimkuta Oscar Pistorius na kosa la kuua bila kukusudia, lakini Ofisi ya Mashitaka haikukubalina na uamzi wa majaji.