Daktari aliyeonya kuhusu virusi vya Corona nchini China afariki dunia
Daktari wa China ambaye alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kutoa taarifa kuhusu mlipuko mpya wa virusi vya Corona amefariki dunia kutokana na maambukizi ya virusi hivyo mapema siku ya Ijumaa, hospitali yake imetangaza.
Imechapishwa:
Li Wenliang Daktari wa magonjwa ya macho amefariki kutokana na maambukizi hayo Ijumaa Alfajiri, Hospitali Kuu ya Wuhan imesema katika taarifa iliyochapishwa kwenye akaunti yake rasmi kwenye jukwaa la mtandao wa kijamii nchini China Weibo.
Kufuatia hatua hiyo, serikali ya China imetangaza kuanzisha uchunguzi maalum kuhusu kifo cha Daktari huyo ambaye ripoti zinasema kuwa, alitishwa alipojaribu kuzungumzia maambukizi hayo hatari.
Kufikia siku ya Ijumaa, watu 630 wamepoteza maisha na wengine 31,000 wameambukizwa kote nchini China.
Rais wa China Xi Jinping na mwenzake wa Marekani Donald Trump ambao wamekuwa wakitofautiana kibiashara, wamezungumzia kuhusu maambukizi ya Corona.
Beijing hata hivyo, imekasirishwa na hatua ya Marekani kuwazuia watu waliotoka nchini China hivi karibuni kutembelea nchi hiyo.