Ndege ya Ukraine: Iran yakataa kutuma visanduku vya kunakili sauti ya ndege nje ya nchi
Wiki mbili baada ya ndege ya Ukraine kudunguliwa na kugharimu maisha ya watu 176 nchini Iran, mamlaka nchini humo ilikubali hivi karibuni kwamba makombora mawili yaliangusha ndege hiyo.
Imechapishwa:
Tehran imekataa kutuma visanduku vya kunakili sauti ya ndege nje ya nchi hiyo.
Wiiki moja iliyopita Canada ilitaka visanduku viwili vya kunakili sauti ya ndege vipelekwe nchini Ukraine au Ufaransa.
Katika ripoti ya awali, mamlaka ya anga nchini Iran ilibaini kwamba makombora mawili yaliyorushwa kimakosa na kusababisha ndege ya Ukraine kuanguka. Ripoti inasema uchunguzi unaendelea kuhusu sababu za shambulio la makombora dhidi ya ndege hiyo.
Mataifa yaliyopoteza raia katika ajali ya ndege ya Ukraine iliyodunguliwa na Iran yameitaka Tehran iwajibike kikamilifu, uchunguzi wa kimataifa uanzishwe na familia za wahanga zilipwe fidia.
Watu wote 176 waliokuwa ndani ya ndege ya abiria ya Ukraine walipoteza maisha yao wakati ndege yao ilipodunguliwa na kombora muda mfupi baada ya kupaa kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Imam Khomeini mjini Tehran tarehe 8 mwezi huu.