Makabiliano makali yazuka kwenye Chuo Kikuu cha Hong Kong
Makabiliano makali kati ya wanafunzi na vikosi vya usalama yaliyozuka tangu Jumapili usiku na kuendelea kwa siku ya leo yamezua wasiwasi mkubwa Hong Kong. Kwa mujibu wa mashuhuda, hali ni tete karibu na Chuo Kikuu cha Hong Kong.
Imechapishwa:
Kila upande unajaribu kukabiliana na mwengine, hali ambayo wadadisi wanasema inatishia mustakabali wa eneo hilo.
Waandamanaji wanajaribu kukimbilia katika maeneo salama baada ya Chuo kikuu cha Hong Kong kuzingirwa na vikosi vya usalama.
Vikosi vya usalama vya Hong Kong vimewashambulia waandamanaji wanaodai demokrasia, ambao walikuwa wakijaribu kutoroka kutoka Chuo Kikuu walichokichoma moto leo, katika mojawapo ya ghasia mbaya kushuhudiwa katika msururu wa maandamano yaliyodumu kwa karibu miezi sita sasa.
Shule zimefungwa, na usafiri wa reli na wa barabara umetatizika kutokana na vizuizi vilivyowekwa na waandamanaji.
Wakati huo huo China ambayo Hong Kong iko chini ya himaya yake imeonya kuwa haitaendelea kuvumilia upinzani wao.
Hayo yanajiri wakati Mahakama mjini Hong Kong leo imeamua kuwa amri tata ya kutofunika nyuso kwa kutumia barakoa wakati wa maandamano ni kinyume na katiba.
Marufuku dhidi ya kufunika nyuso ilitangazwa mwezi Oktoba na kiongozi wa Hong Kong, Carrie Lam, ambaye alianisha lengo lake kuwa ni kusaidia kukabiliana na maandamano ya vurgu yanayoukumba mji huo kwa muda wa miezi kadhaa sasa.