Polisi yashtumiwa kutumia risasi za moto kwa kuwatawanya waandamanaji Hong Kong
Waandamanaji katika eneo la Hong Kong, wamekuwa wakikabiliana na polisi huku ripoti zikisema kuwa mmoja kati ya waandamanaji amepigwa risasi kifuani na wengine zaidi ya 50 kujeruhiwa vibaya.
Imechapishwa:
Makabiliano haya yamekuja, wakati China inapoadhimisha miaka 70 ya chama cha Kikomunisti nchini humo.
Awali, polisi wamekuwa wakitumia risasi za mpira kukabiliana na waandamanaji na hii ndio mara ya kwanza kwa risasi za moto kutumiwa kutuliza maandamano hayo.
Maandamano ya leo yametatiza shughuli za kawaida katika jiji hilo, huku barabara zikifungwa, uahribu mkubwa ukiripotiwa hasa kuharibika kwa majengo.
Kwa muda wa miezi minne maandamano yamekuwa yakiendelea, huku rais wa China Xi Jinping akisema kuwa hakuna anayewezesha kuligawa taifa hilo.
Kila tarehe moja mwezi Oktoba, kumeendelea kushuhudiwa kwa maandamano makubwa dhidi ya serikali ya China, katika eneo hilo ambalo Beijing imekuwa ikiongoza tangu mwaka 1997.
Licha ya Hong Kong kuwa sehemu ya China, waandamanaji mara kwa mara wameendelea kupinga kutawaliwa na China kwa kile wanachokisema kuwa, wanataka kujiongoza na kuendeleza demokrasia.