Indonesia yaomba msaada wa kimataifa kwa kupambana na majanga yanayoikabili
Serikali ya Indonesia inaomba msaada wa Kimataifa baada ya nchi hiyo kushuhudia tetemeko la ardhi na Tsunami katika jimbo la Sulawesu na kusababisha watu zaidi ya 800 kupoteza maisha.
Imechapishwa:
Rais Joko Widodo amesema, nchi yake inapokea msaada wowote kutoka kwa mataifa ya nje na wahisani wema baada ya janga hili baya.
Msaada mkubwa unaohitajika kwa sasa ni dawa, chakula na makaazi kwa wale wote walioathuriwa.
Maafisa nchini humo wanasema watu wengi bado hawajapatikana na kuna uwezekano mkubwa wa idadi ya vifo kuongezeka kwa sababu wengine wamefunikwa na vifusi vya majengo.
Tayari makaburi ya kuwazika zaidi ya watu 800 yamechimbwa ili kuwazika kwa lengo la kuzuia uwezekano wa kusambaa magonjwa katika jimbo hilo.
Tetemeko kubwa lenye ukubwa wa Richter 7.5 lilitokea siku ya Ijumaa na kusababisha majengo kuporomoka huku upepo mkali ukivuma na hata kufika katika mji mkuu wa Palu.