Marekani na Korea Kusini wasitisha mazoezi ya kijeshi
Majeshi ya Marekani na Korea Kusini yametangaza Jumanne wiki hii kwamba wanasitisha mazoezi ya pamoja ya kijeshi yaliyopangwa kufanyika mnamo mwezi Agosti.
Imechapishwa:
Kauli hiyo inakuja siku chache baada ya rais Donald Trump kutangaza kusitishwa kwa mazoezi hayo kufuatia mkutano wake wa kihistoria na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un.
Korea ya Kusini, ambapo kulitumwa maelfu ya askari wa Marekani wanaohusika na kuilinda dhidi ya vitisho vya Korea Kaskazini, imesema kuwa uamuzi huo unahusu mazoezi yanayojulikana kama Ulchi Freedom Guardian.
"Korea ya Kusini na Marekani wanapanga kuendelea na mazungumzo yaokuhusu hatua nyingine," wizara ya ulinzi ya Korea Kusini imesema katika taarifa yake, na kuongeza kwamba "hakuna uamuzi uliochukuliwa kuhusu mazoezi yajayo ".
Takriban askari wa Marekani 17,500 ambao wangelishiriki katika mazoezi hayo ya Freedom Guardian.
"Kulingana na ahadi ya Rais Trump pamoja na mshirika wetu Korea Kusini, jeshi la Marekani limesitisha maandalizi yote ya" michezo ya kivita "kujihami ya mwezi Agosti mwaka huu, Freedom Guardian" amesema Dana White, msemaji wa Pentagon, katika taarifa yake.
Afisa mkuu wa Marekani aliliambia shirika la habari la AFP siku ya Alhamisi kuwa "mazoezi makubwa yamesitishwa kwa muda usiojulikana kwenye peninsula ya Korea."
Mazoezi ya pamoja ya kijeshi yalipangwa kufanyika mwishoni mwa mwezi Agosti-hadi mwanzoni mwa mwezi Septemba, kama ilivyo kila mwaka.