Trump akutana kwa mara ya kwanza na kiongozi wa Korea Kaskazini
Rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa Korea Kaskazini Kim Jong Un wamebadilishana maneno ya busara na kushikana mikono katika tukio la kihistoria wakati huu viongozi hawa wakimaliza awamu ya kwanza ya mazungumzo ya awali nchini Singapore.
Imechapishwa:
Katika siku na tukio ambalo hakuna aliyewahi kufikiri kuwa rais wa Marekani anaweza kuketi kwenye meza moja ya mazungumzo na kiongozi wa taifa la Korea Kaskazini, hatimaye siku na tukio lenyewe vimetimia baada ya rais Donald Trump kukutana na Kim Jong Un.
Baada ya miongo kadhaa ya mvutano, urushianaji maneno makali na ya kejeli kwa miongo kadhaa, hatimaye rais Donald Trump ameshikana mkono na Kim Jong Un katika tukio ambalo limetazamwa na viongozi wa dunia na kuoneshwa kupitia njia ya televisheni.
Alikuwa ni rais Trump ambaye alikuwa wa kwanza kabisa kutoa mkono wake kwa Kim Jong Un ambaye nae alimshika mkono Trump na kupiga picha ya pamoja mbele ya wanahabari zaidi ya elfu 5 walioko Singapore kuripoti mkutano huu.
Wakiwa wameketi sambamba, rais Trump amesema ana imani nchi yake itakuwa na uhusiano mzuri na Korea Kaskazini kupitia mazungumzo yao, huku Kim Jong Un akikiri kuwa haikuwa rahisi kufikia hatua waliyofikia hivi leo na kwamba kukutana kwao tu ni ishara nzuri.