Trump na Kim kukutana Jumanne hii Sentosa
Zimesalia saa chache kabla ya kufanyika kwa mkutano wa kihistoria kati ya rais wa Marekani Donald Trump na kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, wakati huu viongozi wote wawili wakiwa wameshawasili nchini Singapore kwa nyakati tofauti.
Imechapishwa:
Mkutano wao ambao ni wa kwanza utafanyika siku ya Jumanne katika kisiwa cha Sentosa, Singapore.
Miongoni mwa ajenda zinazotarajiwa kujadiliwa na viongozi hawa wawili siku ya Jumanne wiki hii ni pamoja na kufikiwa makubaliano rasmi ya kusitisha vita vya Korea vilivyodumu kwa miaka 65 pamoja na Korea Kaskazini, Pyongyang kuachana na mpango wake wa kurutubisha Uranium kwa kubadilishana na kuondolewa vikwazo na Marekani.
Hata hivyo Marekani ina matumaini kuwa kukutana kwao utakuwa mwanzo wa mchakato ambao hatimaye itashuhudiwa Kim akiachana na mpango wake wa silaha za nuklia.
Maofisa kutoka pande zote mbili wamekuwa wakikutana kwa nyakati tofauti kujadiliana kuhusu taarifa ya pamoja ambayo itatolewa na viongozi hao mwishoni mwa mkutano pamoja na ajenda zenyewe.