Mazungumzo kati ya Korea Kaskazini na Kusini wiki ijayo
Korea Kaskazini imekubali kushiriki katika mazungumzo kati yake na Korea Kusini, yaliyopangwa kufanyika wiki ijayo.
Imechapishwa:
Lengo la mazungumzo kati ya nchi hizi mbili ni kujaribu kupata namna wanamichezo wa Korea Kaskazini watahudhuria michezo ya Olimpiki ya msimu wa baridi, itakayofanyika nchini Korea Kusini mwezi Februari.
Wiki hii, kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un alisema kuwa alikuwa tayari kwa mazungumzo na jirani yake, kwa lengo la kuwawezesha wachezaji wa nchi yake kuhudhuria mashindano hayo.
Mkutano huo unatarajiwa kufanyika katika eneo la Panmunjom, katika mpaka wa nchi hizo mbili, eneo ambalo linaelezwa la kihistoria kati ya nchi hizo mbili.
Mazungumzo ya mwisho kati ya nchi hizi mbili, yalifanyika mwaka 2015. Haijafahamika ni nani watakaohudhuria mazungumzo haya mapya.
Hatua hii, imeonekana kutuliza uhasama kati ya nchi hizi mbili, kutokana na mradi wa Korea Kaskazini kuzalisha silaha za nyuklia.
Korea Kaskazini imekuwa ikitishia kuishambulia Marekani na washirika wake kama Korea Kusini.
Rais wa Marekani Donald Trump amepongeza hatua hiyo ya kuwepo kwa mazungumzo hayo.